Mambo manne ambayo huenda usifunzwe shuleni

Uwe bora kadri ya uwezo wako

Tunajifunza mambo mengi muhimu shuleni: hesabu, sayansi, stadi za kusoma na kuandika, na huo ni mwanzo tu! Lakini kuna mambo ambayo hatufunzwi shuleni ambayo tunajifunza tu kutokana na maisha halisi. Mambo haya ni yapi?

#MALENGO

Tunaona mambo haya kwenye mitandao ya kijamii, sivyo? #MALENGO! Lakini hatupaswi tu kutumia neno hili kurejelea #malengoyawapendanao au #malengoyamazoezi. Badala yake, kila mmoja wetu anapaswa kuwa na #malengo ya kibinafsi. Iwapo una ndoto kuhusu maisha yako ya baadaye, jitahidi kuzitimiza!

Andika malengo ambayo unataka kutimiza katika mwaka unaofuata. Je, ni kujiunga na chuo kikuu? Kuanzisha biashara? Kupata kazi? Hata kama malengo yako ni makubwa, usiogope. Yapange katika hatua ndogo, kisha uanze na lengo linaloweza kutimizwa kwa wepesi zaidi.

Anza kupanga Bajeti

Mojawapo ya kanuni za kimsingi maishani ni: usitumie pesa nyingi kuliko kiasi unachopata. Anza kuhifadhi pesa, hata kiasi kidogo zaidi. Unapofanya uamuzi kununua kitu, tafakari kuhusu iwapo kwa kweli unakihitaji. Wakati mwingine kununua vitu bila mpango au kutumia pesa bila kupangia kunaweza kuwa kizuizi kikuu katika kutimiza #malengo yetu.

Dumisha Afya bora

Kufuata malengo yako sio jambo rahisi na unahitaji kuhakikisha kwamba una nguvu za kukuwezesha kuendelea. Ili mwili wako uwe na nguvu hii, unahitaji kuwa na afya njema. Kufanya mazoezi vilevile hukusaidia kuimarisha akili yako. Ni nafasi yako ya kuimarisha ustahimilivu na mawazo chanya kadri unavyojisukuma ili usikate tamaa hata unapohisi kushindwa.

Wakati ni dhahabu

Umewahi kusikia msemo wa Kiingereza “time is gold?” Unachomaanisha ni kuwa wakati ni kitu cha thamani mno. Hupita haraka na huwezi kuurejesha. Kwa hivyo daima tunapaswa kuwa na busara katika matumizi ya wakati tulionao na kufanya mambo yaliyo na umuhimu zaidi.

Kwa hivyo dada, jiwekee malengo, panga, weka akiba na uchukue hatua! Utakaribia ndoto zako hivi karibuni.

Share your feedback