Nilipata imani...

Kuwa mtu ninayetaka kuwa

Kupata imani ni jambo ambalo hutokea unapoanza kujiamini bila kuhitaji idhini ya mtu yeyote. Unaanza kufahamu uwezo wako mwenyewe na sio kwa sababu ya mambo ambayo wengine wanasema, lakini ni kwa sababu unajua kuwa uwezo na nguvu hizo hutoka ndani ya mtu. Ninalifahamu hili sasa, lakini haijawa hivi kila wakati. Nilipoanza kuwa mtu mzima, nilikuwa mwenye aibu na wasiwasi sana. Ni pale ambapo nilipata ari yangu na kuanza kufanya mambo ambayo ninayapenda kweli ndipo mambo yalipoanza kubadilika upande wangu.

“Papa ndiye kiongozi wa familia”, mamangu aliniambia mimi pamoja na dada zangu wadogo kila mara. “Lolote analosema linakuwa na usiwahi kuzungumza wakati ambapo husemeshwi.” Unaposikiliza maneno hayo mara nyingi utotoni mwako yatafanya uchukue mwelekeo fulani wa kitabia. Nilianza kuamini kuwa kuzungumza kwa uchache kadri iwezekanavyo kungekuepusha kuzungumza mambo yasiyo sahihi na kungekusaidia kuepuka matatizo.

Wakati mwingine walimu na marafiki zangu katika shule ya msingi hawangetambua iwapo nilikuwa darasani kwa sababu sikuwahi kunyanyua mkono wangu au kuzungumza na watu. Ingawaje nilikuwa mwanafunzi mwerevu, hatua ya kuwa mkimya ilimaanisha kuwa nilijitegemea kila wakati na sikuomba msaada wakati nilipouhitaji. Ilimaanisha kuwa walimu hawakuhisi kuwa wangeniamini katika nafasi za uongozi kama vile kiranja mkuu msichana au kiranja wa darasa. Nilitaka kuwa kiranja mkuu msichana, lakini ilikuwa vigumu kujiamini kwa vile sikujiamini katika kuzungumza na nilipofikiri kuwa walimu wangu hawakuniamini pia. Nilizoea kuwa katika hali hiyo na mwishowe ndoto zangu za kuwa kiranja mkuu msichana zikatoweka.

Mambo yalianza kubadilika kweli nilipojiunga na shule ya upili na kujiunga na timu ya soka. Mwalimu mkuu aliwahimiza wasichana zaidi kuanza kucheza michezo ya spoti na nikajiambia, “kwa nini isiwe hivyo?”.

Baada ya mwezi mmoja wa kujiunga, niliweza kuhisi mabadiliko katika nafsi yangu pale nilipoanza kucheza katika uwanja huo wa soka, nilijihisi huru zaidi na nilipenda kujifunza na kudhibiti mwili wangu. Sikujali mawazo ya watu kunihusu nilipokuwa uwanjani! Sikuwa na aibu au mkimya kwa jinsi nilivyokuwa nikisonga nilipokuwa nikicheza soka. Nilijihisi kama nyota uwanjani na nilijihitaji mimi mwenyewe kujua hili.

Pindi timu yetu ilipokuwa tayari kushindana na shule zingine, mkufunzi wangu aliamua kunifanya kuwa nahodha wa timu ya soka! Haikuwa vigumu kuwa nahodha kwa sababu nilijiamini mimi mwenyewe ilipofika wakati wa soka na nilijua kuwa ninaweza kuongoza na kuwasaidia wasichana wengine katika timu yangu. Ilinipa pia imani kuwa muwazi zaidi darasani na kuuliza maswali nilipohitaji kufanya hivyo. Jambo bora zaidi kuhusu imani ni kujua kuwa haijalishi kuwa uko sahihi au la kuhusu jambo lolote. Jambo la muhimu ni kujaribu kuwa mtu bora zaidi!

Kwa hiyo vidokezo vyangu vikuu vya kuwa na imani zaidi ni vipi?

  1. Mbinu rahisi ya kuweza kujiamini kwa ndani ni kuhisi mwenye nguvu kwa nje. Chukua muda wa kujinyoosha na kuinua kichwa chako juu.
  2. Wito ni sentensi moja au mbili ambazo hukusaidia kupata nguvu. Wito wangu ni ‘Ninajitoa kutoka kwenye hali niliyoizoea ili nitimize ndoto zangu’.
  3. Nilijifunza kwamba wakati mwingine, ninahitaji kuomba msaada. Iwapo kuna jambo ambalo linakuvutia, tafuta mtu ambaye anajua maelezo yote kolihusu. Wanaweza kukusaidia kujitayarisha na kushiriki.
  4. Jaribu kufanya jambo jipya unapoweza kufanya hivyo. Haya yanaweza kuwa mambo madogo kweli, lakini yatakusaidia kujiondoa katika hali oliyozoea.

Je, una ari au uraibu ambao ulikusaidia kujiamini? Tueleze hapa chini!

Share your feedback